Saturday, June 30, 2012

Pinda: Tunachunguza bilioni 300 za Uswisi



 WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema Serikali kupitia vyombo vyake vya dola, imeanza kuchunguza taarifa za kuwapo kwa Sh300 bilioni zilizofichwa nchini Uswisi.Pinda aliliambia Bunge jana kuwa, Serikali pia ilisoma taarifa kwenye vyombo vya habari kama walivyosoma wabunge, na kwamba tayari wameanza uchunguzi kuhusu suala hilo na baada ya uchunguzi matokeo yatatangazwa.

Alivitaja vyombo vinavyochunguza tuhuma hizo kuwa ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Taasisi ya Kuchunguza na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Kitengo cha Kiiteliejensia cha Wizara ya Fedha (Fiu).

Pinda aliyasema hayo jana wakati akijibu hoja za baadhi ya wabunge, ambao katika kuchangia bajeti ya Waziri Mkuu walitaka kupewa maelezo ya kutoroshwa kwa fedha hizo.

Taarifa za kufichwa kwa fedha hizo kwenye akaunti sita za wanasiasa na vigogo wa Serikali, ziliripotiwa wiki iliyopita na magazeti ya Mwananchi na The Citizen pekee, zikinukuu ripoti ya Benki ya Taifa ya Uswisi (SNB), iliyotolewa hivi karibuni, ikitaja nchi mbalimbali ikiwamo Tanzania, na kiwango cha fedha zilizohifadhiwa huko.
Mbali ya Tanzania, nchi nyingine ambazo zina fedha nyingi katika benki za Uswisi ni Kenya (Dola 857 milioni), Uganda (Dola 159 milioni), Rwanda (Dola 29.7 milioni) na Burundi Dola 16.7 milioni.

Chanzo cha habari hizo kilieleza kuwa, tangu akaunti hizo zifunguliwe na kampuni za kuchimba mafuta na madini, wamiliki wake halali kutoka hapa nchini, hawajawahi kuingiza hata shilingi moja.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, akichangia bajeti ya Waziri Mkuu, aliitaka Serikali kuchunguza, kuwataja na kuwachukulia hatua wamiliki wa akaunti hizo.
 
Alisema, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ielekezwe ili ifanye uchunguzi utakaowezesha wamiliki wa akaunti zao kufahamika ili wachukuliwe hatua mara moja bila kujali nafasi wanazozishika serikalini.

Jana akijibu hoja za wabunge, Pinda alisema: “Serikali kupitia vyombo vyake (Takukuru, Financial Intelligency Unit (Fiu) wameanza kufanya uchunguzi wa taarifa hizo kwa kuzingatia taratibu za kisheria.”

Pinda pia alionya ukiukwaji wa makusudi wa sheria, taratibu na miongozo mbalimbali ya Serikali, unaofanywa na baadhi ya viongozi wa Serikali wasio waaminifu wakati wa kutekeleza majukumu yao.
“Kwa kweli hatuwezi kuendelea kuvumilia hali hiyo, na sisi tunasema wabunge kupitia kamati zetu zile tatu za masuala ya fedha na kamati nyingine za kisekta mnatusaidia sana maana lazima tubadilike ili tuweze kutoka hapa tulipo,”alisema Pinda.

Pinda alisema Serikali haijalifumbia macho suala hilo na kwamba hatua stahiki za kinidhamu zimekuwa zikichukuliwa kwa viongozi na watendaji wa aina hiyo kila walipobainika.

“Mathalan katika kipindi cha mwaka 2011/2012 wakurugenzi wapatao 48 walichukuliwa hatua za kinidhamu au kufikishwa mahakamani kwa makosa mbalimbali ya kinidhamu ikiwa ni pamoja na vitendo vya wizi, rushwa, ubadhirifu, ukiukaji wa maadili na kushindwa kutekeleza majukumu yao,” alisema Pinda.
Pinda pia alizungumzia kwa undani mgawanyo wa fedha za rada zilizorejeshwa kutoka Uingereza, maarufu kama chenji ya rada, kuwa zitatumika kwa ununuzi wa vitabu na madawati, kwa kuwa ndiyo makubaliano yaliyofikiwa na pande husika.

Pande hizo ni Serikali kupitia Wizara ya Fedha, wakati Uingereza iliwakilishwa na DFID, BAE Systems na SFO.

“Matumizi ya fedha hizo yanalenga kuimarisha uendeshaji wa Elimu ya Msingi ambapo asilimia 75 ya fedha zitatumika kununua vitabu vya kiada, vitabu vya mwongozo kwa walimu, mihutasari na miongozo ya mihutasari, asilimia 25 itatumika kununua madawati,” alisema Pinda.
Alisema vitabu hivyo vitanunuliwa kutoka kampuni 13 za wachapishaji zilizoteuliwa ambazo, ni Ben Company, Best Deal Publisher, E & D Vision, Education Books Publisher, Jadida, LongHorn, Longman, Macmillan, Mkuki na Nyota, Mture, Oxford, Taasisi ya Elimu Tanzania na Ujuzi Book.

Pinda aliongeza kuwa kati ya kampuni hizo, kinyume na ilivyodaiwa na baadhi ya wabunge, mbili tu ndiyo za nje, lakini zina matawi hapa nchini na kwamba kampuni nyingine zilizobaki wamiliki wake ni Watanzania.

No comments: